Tuesday, November 13, 2012

WAZIRI MAGUFULI APONGEZA WAANDISHI KWA KUCHANGIA KUKARABATIWA KWA KIPANDE CHA BARABARA IRAMBA

 Waziri wa ujenzi Dkt. John Pombe Magufuli akikagua kipande cha barabara (kilometa 33) zinazorudiwa kujengwa kwa kiwango cha lami na kampuni ya CHICO ambayo inadaiwa awali kuijenga chini ya kiwango. Kampuni ya CHICO inajenga kipande hicho kwa gharama zake pamoja na mkandarasi mshauri. Gharama ya ujenzi wa kipande hicho kinachoanzia katika kijiji cha Misigiri hadi Shelui ni zaidi ya shilingi bilioni 80.

 Meneja wa TANROADS mkoa wa Singid Mhandisi Yustaki Kangole akitoa taarifa yake ya ujenzi wa kipande cha barabara kinachoanzia kijiji cha Misigiri hadi Shelui kilometa 33. Kipande hicho kinarudiwa kujengwa na kampuni ya kichina CHICO baada ya awali kukijenga chini ya kiwango.

 Waziri wa ujenzi Dkt. John Pombe Magufuli (wa kwanza kushoto) akiwa na mkuu wa mkoa wa Singida Dkt. Parseko Kone (katikati) na Mkuu wa wilaya ya Iramba Yahaya Nawanda (wa kwanza kulia). Muda mfupi kabla ya waziri Magufuli kuzungumza na wafanyakazi wa kampuni ya CHICO.   

Dkt. John Pombe Magufuli akizungumza na wafanyakazi (hawapo kwenye picha) wa kampuni ya CHICHO inayorudia kujenga kipande cha kilometa 33 kinachoanzia kijiji cha Misigiri hadi Shelui wilayani Iramba.
Waziri wa Ujenzi Dkt. John Pombe Magufuli amewapongeza waandishi wa habari kwa juhudi zao za kutangaza/kuandika bila kuchoka habari za ubovu wa kipnade cha barabara kuu cha mlima  Sekenke wilayani Iramba.
Amesema juhudi hizo za kuanika hadharani ubovu wa kipande hicho na madhara yake, zimechochea serikali kulazimisha kampuni ya CHICO, kurudia kwa gharama zake kukijenga upya kipande hicho chenye urefu wa kilomita 33.3.
Dkt. Magufuli ametoa pongezi hizo wakati akizungumza kwenye kikao cha pamoja cha wafanyakazi wa kampuni ya CHICO na viongozi mbali mbali wa seriklai mkoa wa Singida.
Amesema kazi ya kulazimisha kampuni ya CHICO kurudia kukijenga kipande hicho, haikuwa rahisi kwa madai kwamba ilikwisha kabidhi barabara hiyo baada ya kipindi kilichowekwa kisheria cha uangalizi wa ubora wa barabara (defect liability period) kukamilika Januari mwaka 2009.
Magufuli amesema pamoja na kukabidhi barabara hiyo, haikuchukua miezi miwili kipande hicho cha barabara kilibainika kujengwa chini ya kiwango, baada ya kuanza kuharibika kwa kasi.
Akifafanua zaidi, Waziri huyo amesema uharibifu huo ulipigiwa kelele sana na watu mbali mbali, wakiwemo waandishi wa habari.
Kwa upande wa Makandarasi na makandarasi washauri kujenga barabara chini ya kiwango, amesema serikali haitawavumilia makandarasi wa aina hiyo, itawanyang’anya kazi waliyopewa.
Aidha, Magufuli alisema wakurugenzi watendaji wa halmashauri watakaotumia vibaya fedha za mfuko wa barabara, nao watajibishwa.
Katika hatua nyingine, waziri Magufuli ameipa kampuni ya CHICO miezi mitatu kuhakikisha imemaliza ujenzi huo wa kilomita 33.3, vinginevyo hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi ya kampuni hiyo.
Kwa upande wake meneja wa site wa CHICO Stone Chene, amesema kazi hiyo itawagharimu CHICO zaidi ya dola za kimarekani milioni tano.

No comments:

Post a Comment