Wednesday, October 23, 2013

AUAWA NA KUFUKIWA KWENYE SHIMO LA KINA KIFUPI,FISI WAMFUKUA NA KUMBAKIZA MIFUPA.

Jeshi la Polisi Mkoani Singida limefanikiwa kupata mabaki ya mifupa ya mtu anayedhaniwa kuwa ni Saidi Ngereza (35) mkazi wa Dominiki wilaya ya Mkalama.

Inadaiwa Septemba 30 mwaka huu saa 2.30 usiku Saidi alimuaga mke wake Aziza Khamisi (22) kuwa anakwenda kwa jirani yake kwa ajili ya kumjulia hali kwa vile alikuwa akiumwa.

Habari zaidi zinadai kuwa toka siku hiyo aliyoaga hakurudi nyumbani kwake hadi oktoba 14 mwaka huu saa 6.00 mchana makaki ya mifupa yake yalipogunduliwa hatua kilomita tatu toka nyumbani kwake.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida, ACP Geofrey Kamwela amesema mke wa Saidi, Aziza,aliweza kutambua kuwa mabaki ya mifupa hiyo ni ya mume wake kutokana na nguo zilizokutwa karibu na mabaki ya mifupa hiyo.

“Aziza alitambua nguo hizo ambazo ni suruali ya jeans na bukta nyeusi alizovaa mume wake siku ya Septemba 30 wakati anaaga kwenda kwa jirani kumjulia hali”,alifafanua Kamwela.

Aidha amesema baada ya mabaki ya mifupa hiyo kufanyiwa uchunguzi na daktari ilionekana kuwa
marehemu Saidi alipigwa na kitu kizito kichwani na pia kukatwa na kitu chenye ncha kali kichwani.

“Uchunguzi wa awali wa polisi pia unaonyesha kuwa mara baada ya mtu huyo Saidi kupigwa na kuuawa alifukiwa kwenye shimo lenye kina kifupi Fisi waliweza kufukua mwili huo kutokana na harufu kali na kuula na kubakisha mifupa”,amesema Kamwela.

Kamanda Kamwela amesema kwa sasa wanawashikilia watu wawili kwa mahojiano kuhusiana na mauaji hayo.Kwa sasa hatuwezi kutaja majina ya watu tunaowashikilia kwa sababu kitendo hicho kinaweza kuvuruga upelelezi.

Hata hivyo amesema mtuhumiwa mmoja ambaye Saidi (marehemu) aliaga kuwa anaenda kwake kumjulia hali baskeli ya marehemu aliyoondoka nayo ilikutwa kwake.

No comments:

Post a Comment