Friday, January 10, 2014

Watu watatu wa familia moja wamefariki dunia baada ya kugongwa na basi la Mtei Express.

Basi la kampuni ya Mtei Express T.742 ACU linavyoonekana baada ya kuchomwa moto na wananchi wenye hasira kali wa kitongoji cha Ijanuka kijiji cha Kisasida manispaa ya Singida,kutokana na kugonga pikipiki aina ya sky go T.368 BXZ na kuua abiria watatu waliokuwa kwenye pikipiki hiyo.Basi hilo lilikuwa likitoka Singida mjini kuelekea Arusha mjini leo.

 WATU watatu wa familia moja wamefariki dunia baada ya pikipiki waliyokuwa wakisafiria kugongwa na kuburutwa na basi la kampuni ya Mtei Express ya mjini Arusha.

Watu hao ni Tamili Shaban na Kassimu wamefariki dunia papo hapo kwenye eneo la tukio ambalo ni kitongoji cha Ijanuka kijiji cha Kisasida Manispaa ya Singida.Hamza amefariki dunia akiwa anaendelea kupatiwa matibabu katika hospitali ya mkoa mjini Singida.Miili ya watu hao imehifadhiwa katika chumba cha mochwari katika hospitali ya mkoa.


Baba mzazi wa watoto hao,Shaban Bunku ambaye imedaiwa ni mlinzi wa kampuni ya TTCL mjini hapa,amelazwa katika hospitali ya mkoa na hali yake ni mbaya.Inadaiwa kuvunjika mguu wa kulia na damu zilikuwa zikimtoka kichwani.

Wanafamilia hao wanadaiwa walikuwa wakienda shamba kuendelea na palizi.

Akizungumzia tukio hilo la kusikitisha,Kamanda wa Polisi Mkoa wa Singida,SACP Geofrey Kamwela amesema tukio hilo limetokea leo saa moja na dakika moja asubuhi huko katika kitongoji cha Ijanuka kijiji cha Kisasida.

Amesema siku ya tukio,basi la kampuni ya Mteni lenye namba za usajili T.742 ACU aina ya scania likiendeshwa na Dismas Ludovick,lilikuwa linatokea Singida mjini likielekea Arusha mjini.

Kamwela amesema lilipofika kitongoji cha Ijanuka,kwa  pikipiki aina ya sky go T.368 BXZ iliyokuwa inaendeshwa na Shaban Bunku huku akiwa amepakia watoto wake wa kiume watatu,ilikatisha ghafla kitendo kilichosababisha kugongwa na kuburutwa zaidi ya hatua 20.

“Dereva wa basi hilo ambalo lilikuwa na abiria tisa,alilazimika kusimamisha basi hilo kutokana na kuburuta pikipiki hiyo.Baada ya kusimamisha basi hilo,wananchi wa eneo hilo walipigiana simu na ghafla walijaa na kuanza kuvunja vunja vyoo na kisha kilichoma moto”,amesema Kamwela.

Wakati huo huo,Kamanda Kamwela amesema wameanzisha msako mkali wa kusaka

wananchi waliojichukulia sheria mkononi ili kuwakamata waweze kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.

“Tabia hii ya kujichukulia sheria mkononi haikubaliki,tutahakikisha tumewakamata wote waliohusika na uharibifu huu.Sheria ipo wazi kwamba hata kama mtu kafanya kosa,wananchi hawaruhusiwi kabisa kujichukulia sheria mkononi”,alifafanua.

No comments:

Post a Comment