Thursday, February 20, 2014

Mbaroni kwa kukutwa na meno ya Tembo.

                    Kamanda wa Polisi mkoa wa Singida, SACP Geofrey Kamwela.

JESHI la Polisi Mkoa wa Singida limefanikiwa kumkamata George James (30) mkazi wa kijiji cha Mwamagembe tarafa ya Itigi wilaya ya Manyoni mkoa wa Singida kwa tuhuma ya kumiliki kinyume cha sheria nyara za serikali vipande 21 vya meno ya tembo.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Singida,SACP Geofrey Kamwela amesema wamefanikiwa kumkamata George februari 13 mwaka huu saa 2.30 asubuhi huko katika kizuizi cha mazaoa ya misitu na chakula kilichopo katika kijiji cha Ukimbu kata ya Mgandu,tarafa ya Itigi,wilaya ya Manyoni.

Amesema mtuhumiwa huyo alikuwa akitumia gari aina ya toyota hieze T.797 CQL kusafirisha nyara hizo kutoka kijiji cha Mwamangembe kwenda Itigi mjini.

“Baada ya kufanya upekuzi makini,vijana wangu waliweza kuzikuta nyara hizo zikiwa kwenye
mabegi mbalimbali yanayotumika kuhifadhia nguo kana kwamba alikuwa amebeba nguo tu”,alifafanua.

Kamwela amesema uchunguzi wa awali wa polisi ukishirikisha idara ya wanyapori,umeonyesha kuwa vipande hivyo 21 vinakadiriwa kuwa vya tembo wanne,vina uzito wa kilogramu 49 na thamani ya zaidi ya shilingi 43.1 milioni.

Katika tukio jingine,Kamanda huo amesema kuwa wanawashikilia watu watatu kwa tuhuma ya kumiliki misokoto 192 ya bhangi.

Kamwela aliwataja watu hao kuwa ni Nuru Saimon (38) mkulima mkazi wa Njia panda,Williad Kajuna (45) na Said Juma (20) wote wawili wakulima na wakazi wa Majengo Singida mjini.mkazi.

Amesema watu hao wamekamatwa februari 11 mwaka huu huko katika maeneo ya njia panda kata ya Mughunga tarafa ya Ilongero wilaya ya Singida.

“Baada ya taarifa ya raia mwema kutufikia kuwa katika nyumba ya mtuhumiwa Nuru kuwa kuna bhang,ndipo askari hao walipofika katika nyumba hiyo na kufanya upekuzi ndani ya nyumba ambapo waliikuta bhangi hiyo ikiwa ndani ya begi”,amesema Kamwela.

No comments:

Post a Comment