Friday, April 11, 2014

SACCOS Singida yatoa zaidi ya shilingi 329 milioni.

Mwenyekiti wa chama cha ushirika cha akiba na mikopo cha RS SACCOS Ltd, Mkoa wa Singida,Samson Ntuga akiwa ofisini kwake akitekeleza majukumu yake ya kila siku.Wanachama wa SACCOS hiyo ni watumishi wa katibu tawala mkoa wa Singida iliyochini ya ofisi ya mkuu wa mkoa.

CHAMA cha ushirika cha akiba na mikopo cha RS SACCOS ltd,mkoani Singida kimetoa mikopo mbali mbali yenye thamani ya zaidi ya shilingi 329 milioni kwa kipindi cha kati ya mwaka 2008 na mwaka huu.

Hayo yamesemwa hivi karibuni na mwenyekiti wa chama hicho, Samson Ntunga wakati akitoa taarifa yake ya mwaka mbele ya mkutano mkuu wa mwaka uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa ofisi ya mkuu wa mkoa mjini hapa.

Amesema mikopo hiyo midogo na mikubwa imeweza kuwasaidia wanachama ambao ni watumishi wa ofisi ya katibu tawala mkoa wa Singida kupunguza makali ya maisha.

Akifafanua zaidi, Ntunga amesema kuwa mikopo hiyo imewawezesha wanachama hao kugharamia masomo ya watoto wao,ujenzi wa nyumba na kuongeza mitaji kwa ajili ya miradi/biashara zao.

“Katika mafaniko mengine,chama kimebuni mradi wa viwanja kwa ajili ya wananchama vya gharama nafuu.Wakati wo wote kuanzia sasa tunatarajia wanachama wetu wapatao 222 kila mmoja atakabidhiwa
kiwanja chake na zoezi hilo litaingiza mapato ya shilingi 55 milioni kwa chama chetu”,alisema.

Katika hatua nyingine,Mwenyekiti huyo alitaja baadhi ya changamoto wanazokabiliana nazo kuwa ni mtaji mdogo usiokidhi mahitaji ya wanachama kucheleweshwa kwa makato (deductions) na baadhi ya wanachama kutaka kukopa kinyume na sheria ya vyama vya ushirika na.20 ya mwaka 2003.

“Tatizo la kucheleweshwa kwa makato yatokanayo na mishahara, linachangia ucheleweshaji wa utoaji wa mikopo kwa wananchama.Ili kulitatua tatizo hilo chama kinatarajia kuingia mkataba na hazina ili makato ya kila mwezi yaingizwe moja kwa moja kwenye akaunti ya chama bila kupitia kwa mwajiri”, alifafanua.

SACCOS hiyo inatarajia kukusanya mapato ya zaidi ya shilingi 136 milioni kutoka kwenye vyanzo vyake mbalimbali vya mapato,kwa mwaka wa fedha wa mwaka huu wa 2014.Pia inatarajia kutumia zaidi ya shilingi 76.2 milioni.

No comments:

Post a Comment