Wednesday, November 26, 2014

Mazingira yasiyo rafiki yakwamisha masomo mabinti wanaobalehe.

Kaimu mkuu wa mkoa wa Singida na mkuu wa wilaya ya Iramba,Yahaya Nawanda,akizungumza kwenye kilele cha maadhimisho ya siku ya kunawa mikono duniani, matumizi ya vyoo bora duniani na usafi wa mazingira kwa mkoa wa Singida.Maadhimisho hayo yamefanyika katika kijiji cha Mgongo kata Shelui wilaya ya Iramba.
Kaimu mkuu wa mkoa wa Singida na mkuu wa wilaya ya Iramba,Yahaya Nawanda,akimpongeza meneja wa shirika la SEMA, Ivo Manyanku (aliyekaa) kwa kazi nzuri ya kuhamasisha wananchi wa wilaya ya Iramba kujenga vyoo bora na kuvitumia.

Meneja wa shirika la SEMA, Ivo Manyanku akizungumza kwenye  kilele cha maadhimisho ya siku ya kunawa mikono duniani, matumizi ya vyoo bora duniani na usafi wa mazingira kwa mkoa wa Singida.Maadhimisho hayo yamefanyika katika kijiji cha Mgongo kata Shelui wilaya ya Iramba.Kulia ni kaimu mkuu wa mkoa wa Singida na mkuu wa wilaya ya Iramba,Yahaya Nawanda.
Baadhi ya wakazi wa kata ya Mgongo kata ya Shelui wilaya ya Iramba, waliohudhuria  kilele cha maadhimisho ya siku ya kunawa mikono duniani,matumizi ya vyoo bora duniani na usafi wa mazingira kwa mkoa wa Singida.

WANAFUNZI  wa kike ambao wamefikia umri wa kubalehe, kipindi  cha hedhi hulazimika kuacha masomo  na kukaa nyumbani takribani siku 60 za masomo kwa mwaka; imeelezwa

Imedaiwa hali hiyo kwa kiasi kikubwa, inachangiwa na ukosefu wa mazingira rafiki shuleni kwa wanafunzi wa kike waliobalehe.

Hayo yamesemwa na mkuu wa Mkoa wa Singida, Dk. Parseko Kone, wakati akizungumza kwenye kilele cha maadhimisho ya siku ya kunawa mikono duniani, siku ya matumizi ya choo duniani na wiki ya usafi wa mazingira kimkoa, yaliyofanyika katika kiiji cha Mgongo Wilayani Iramba.


Alisema tafiti za kisayansi zinathibitisha kuwepo kwa uhusiano wa ongezeko la mahdhurio ya wanafunzi shuleni linalochangiwa na uboreshaji wa miundombinu ya maji na usafi wa mazingira, katika shule husika.

“Katika shule ambazo hazina miundo mbinu ya maji na usafi wa mazingira, hali huwa mbaya mno kwa wanafunzi wa kike waliobalehe. Hali hii huwalazimu kukaa nyumbani kipindi chote wanachokuwa katika hedhi, huku masomo shuleni yakiwa yanaendelea”,alifafanua katika hotuba yake iliyosomwa kwa niaba yake na mkuu wa wilaya ya Iramba,Yahaya Nawanda.

Akisisistiza, alisema kwa wastani kwenye  shule zisizo  na miundo mbinu rafiki kwa wasichana kama maji safi, vyoo bora na vichomea ‘pad’, msichana husika  hupoteza takribani siku 60 za masomo kila mwaka.


“Hii inamaana  kuwa tunahitajika kuboresha hali ya usafi na mazingira pamoja na miundombinu muhimu  katika shule zote, ili matokeo makubwa sasa yaweze kifikiwa katika sekta ya elimu”,alisisitiza zaidi.

Katika hatua nyingine,Dk. Kone ametoa wito kwa jamii kushirikiana na Serikali kuhakikisha kila shule inakuwa na huduma ya vyoo bora pamoja na sehemu maalumu za kunawa mikono, ili kuwakinga wanafunzi  dhidi ya maradhi yanayoenezwa kwa njia ya uchafu.


Mkuu huyo wa mkoa alitumia fursa  hiyo kuyashukuru mashirika ya siyo ya kiserikali ya Water Aid Tanzania  na SEMA kwa mchango wao wa hali na mali ambao umefanikisha kwa kiwango cha juu maadhimisho ya mwaka huu.

No comments:

Post a Comment