Friday, January 2, 2015

Mwendesha bodaboda atekwa na kuchinjwa Singida.

Kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa Singida, ACP, Thobias Sedoyeka.

WATU watatu mkoani Singida,wamefariki dunia katika matukio tofauti, likiwemo la dereva wa boda boda kuchomwa kisu shingoni na usoni juu ya jicho la kushoto.

Kamanda wa jeshi la polisi Mkoa wa Singida,ACP,Thobias Sedoyeka,alimtaja dereva wa boda boda aliyechomwa kisu na kufariki dunia,kuwa ni Sudi Jumanne (26) mkazi wa Sabasaba mjini hapa.

Alisema mwili wa dereva Sudi uliokotwa na raia wema Novemba 22 mwaka huu saa moja asubuhi,huko maeneo ya uwanja wa ndege mjini hapa.

 Sedoyeka alisema Sudi alichomwa kisu na mtu/watu wasiofahamika shingoni karibu na bega la kushoto na usoni juu ya jicho la kushoto.

Kamanda huyo alisema katika tukio la pili,Kundi Oshima (75) mkulima na mkazi wa kijiji cha Iyumbu wilaya ya Ikungi,amefariki dunia baada ya kukatwa katwa mapanga kisogoni, shavu la kushoto na mtu/watu wasiofahamika.

Alisema tukio hilo limetokea Novemba 22 mwaka huu saa saba usiku huko katika kijiji na kata ya Iyumbu tarafa ya Ihanja wilaya ya Ikungi.

“Uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa chanzo cha mauaji hayo,ni imani ya kishirikina.Kwa sasa tunamshikilia Dalush Mwandu (51) kwa mahojiano zaidi”,alisema.

Sedoyeka alisema pia Novemba 23 mwaka huu saa 10.20 jioni huko katika maeneo ya bwawa Singidani mjini hapa,kitoto kichanga kinachokadiriwa kuwa na umri wa siku mbili cha kiume,kimeokotwa kikiwa kimefariki dunia.

“Chanzo cha kutupwa kwa motto huyo,bado hakijajulikana na hakuna mtu/watu waliokamatwa kuhusiana na tukio hilo”.alisema kamanda Sedoyeka.

No comments:

Post a Comment