Tuesday, November 11, 2014

TUNAJALI wawajali wanawake na vifaa tiba vya mil 155/-

Mkurugenzi wa shirika lisilo la kiserikali la TUNAJALI, Dk.Gottlieb Mpangile (kushoto) akizungumza kwenye hafla ya kuzindua mpango wa kutokomeza vifo vya wajawazito na watoto wachanga mkoani Singida, Pia hafla hiyo ilitumika kutoa msaada wa vifaa tiba vikiwemo vitanda vya kujifungulia vyote kwa pamoja  vikiwa na thamani ya zaidi ya shilingi 155 milioni.Wa pili kushoto (waliokaa) ni mkuu wa mkoa wa Singida, Dk.Parseko Kone na wa kwanza ni katibu tawala mkoani Singida, Liana Hassan.
Mkuu wa mkoa wa Singida, Dk.Parseko Kone, akizungumza kwenye hafla ya kuzindua mradi wa kutokomeza maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto na kukabidhiwa vifaa tiba na shirika la TUNAJALI. Wa kwanza kushoto ni Katibu Tawala mkoa wa Singida, Liana Hassan na Kulia ni Mkurugenzi wa shirika la TUNAJALI, Dk. Gottlieb Mpangile.

Mkuu wa mkoa wa Singida, Dk.Parseko Kone (katikati) akizindua mradi wa kutokomeza maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto. Kulia ni mkurugenzi wa TUNAJALI,DK.Gottlieb Mpangale na Kushoto ni Katibu Tawala mkoa wa Singida,Liana Hassan.
Mkuu wa mkoa wa Singida, Dk.Parseko Kone (katikati) akiwa ameshikilia bango lenye ujumbe wa kutokomeza maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto. Kushoto ni Katibu Tawala mkoa wa Singida, Liana Hassan na kulia ni Mkurugenzi wa TUNAJALI, Dk.Gottlieb Mpangile.
Afisa taaluma wa TUNAJALI, Dk.Asnath Nnko (kushoto mwenye miwani) akimwonyesha Mkuu wa mkoa wa Singida Dk. Parseko Kone (wa pili kushoto) baadhi ya vifaa tiba vilivyotolewa msaada na shirika la TUNAJALI kwa hospitali tatu na vituo saba vya mkoa wa Singida.
Mkuu wa mkoa wa Singida, Dk.Parseko Kone, akipewa maelezo dawa mbalimbali kwenye kibanda cha shirika la TUNAJALI.
Baadhi ya wadau wa sekta ya afya waliohudhuria hafla ya kukabidhi vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi 155 milioni vivyotolewa msaada na shirika la TUNAJALI kwa vituo vya afya saba na hospitali tatu.

SHIRIKA lisilo la kiserikali la TUNAJALI, limetoa msaada wa vifaa tiba mbalimbali vyenye thamani ya shilingi 155 milioni, kwa vituo 10 vya afya mkoani Singida kwa ajili ya kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga.

Hayo yamesemwa na mkurugenzi wa TUNAJALI, Dk.Gottlieb Mpangile,wakati akizungumza kwenye hafla ya kukabidhi vifaa hivyo iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa kanisa la katoliki mjini Singida.

Alisema vifaa hivyo ambavyo ni pamoja na vitanda na vifaa vya kujifungulia,vimetolewa na watu wa Marekani kupitia shirika lao la misaada la USAID, ikiwa ni mpango wa dharura wa Rais wa Marekani wa kupambana na UKIMWI (PEPFAR).

Alisema kuwa msaada huo unafuatia tathimini iliyofanywa na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii hivi karibuni mkoani Singida na kugundua upungufu mkubwa wa vifaa tiba katika vituo vya kutolea huduma za afya.

Akifafanua zaidi, Dk.Mpangile alisema vifaa hivyo vitachangia juhudi za Serikali katika kupunguza vifo vya akina mama vitokanavyo na matatizo ya ujauzito,uzazi na vile vya watoto wachanga.Vifo hivyo bado ni tatizo nchini, mkoa wa Singida ukiwemo.

Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Singida ambaye alikuwa mgeni rasmi katika makabidhiano hayo,Dk.Parseko Kone,alisema wajawazito 454 kati ya 100,000,hufariki kutokana na matatizo wakati wa mimba au uzazi.

Aidha,Dk.Kone alisema watoto wachanga 26/1000 hufariki dunia kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ya magonjwa yanayoweza kutibika.

“Hii ni sawa na wakina mama 8,100 na watoto 48,412 hupoteza maisha kila mwaka kutokana na magonjwa ambayo mengi yanatibika”,alisema mkuu huyo wa mkoa.

Alisema serikali ya Tanzania inaazimia kupunguza vifo vya uzazi hadi kufikia 193/100,000 na vya watoto wachanga hadi kufikia 19/1,000 ifikapo mwakani.

No comments:

Post a Comment