Thursday, May 7, 2015

Fedha za TASAF Mkalama Singida wanaume wazipora na kunywea pombe.

Mwenyekiti wa kijiji cha Mwanga tarafa ya Nduguti wilaya ya Mkalama mkoa wa Singida, Jackson Mkoma, akifungua mkutano wa tathmini ya matumizi ya fedha za TASAF awamu ya nne uliofanyika kwenye viwanja vya ofisi ya kituo cha kilimo cha kijiji hicho.
Mratibu wa TASAF wilaya ya Mkalama, Athumani Jumanne Dulle, akizungumza kwenye  mkutano wa tathimini ya matumizi ya fedha za TASAF awamu ya nne uliofanyika kwenye viwanja vya ofisi ya kituo cha kilimo cha kijiji hicho.

 Mmoja wa walengwa wa mradi wa kunusuru kaya maskini kijiji cha Mwanga wilaya ya Mkalama, akizungumza kwenye  mkutano wa tathmini ya matumizi ya fedha za TASAF awamu ya nne uliofanyika kwenye viwanja vya ofisi ya kituo cha kilimo cha kijiji hicho.
Mmoja wa wanufaikaji wa mradi wa kunusuru kaya maskini mkazi wa kijiji cha Mwanga tarafa ya Nduguti wilaya ya Mkalama mkoa wa Singida, Agnes Samson,akionyesha mradi wa Mbuzi aliouanzisha kwa fedha za TASAF.Nyuma yake ni mratibu wa TASAF wilaya ya Mkalama, Athumani Jumanne Dulle.
Familia Yeremia Lyanga, wakazi wa kijiji cha Mwanga wilaya ya Mkalama wakiwa nje ya nyumba yao mpya walioijenga kwa kutumia fedha za TASAF.

BAADHI ya wanaume wa kijiji cha Mwanga tarafa ya Nduguti  wilaya ya Mkalama mkoani Singida, wametuhumiwa kuwanyang’anya wake zao fedha za mradi wa kunusuru kaya maskini sana zinazotolewa na TASAF,na kuzitumia kunywea pombe, kitendo kilichodaiwa kukwamisha malengo na madhumini ya maradi huo.

Hayo yamesemwa na walengwa wa mradi huo awamu ya nne katika kijiji hicho,waliohudhuria mkutano ulioitishwa kwa ajili ya kufanya tathimini ya matumizi ya fedha zilizotolewa na TASAF kwa kaya masikini sana hivi karibuni.

Walisema pamoja na ruzuku hizo zinazotolewa na TASAF kuonyesha mafanikio makubwa kwa kuzikomboa kiuchumi kaya nyingi maskini katika kijiji hichobaadhi ya wanaume wamekuwa wakorofi kwa kunyang’anya wenza wao fedha hizo na kuzitumia kunywea pombe,kuongeza wake na matumizi mengine ambayo yapo, kinyume ma madhumuni na malengo ya TASAF,na hivyo kuendeleza umaskini katika kaya husika.

Ushuhuda uliotolewa kwenye mkutano huo,ulidai kuwa mwanaume mmoja (jina tunalo) alipokea ruzuku ya shilingi 44,000 kwa niaba ya mke wake (mwanamke ndiye aliyeandikishwa kwenye daftari la walengwa) ambaye kwa wakati huo alikuwa mgonjwa taabani.

Inadaiwa baada mwanaume huyo kuchukua ruzuku hiyo, hakurejea nyumbani kwake na badala yake alishinda kijiji jirani cha Mwando akitumia fedha za TASAF kunywea pombe na kununua viatu vya watoto wake aina ya bajaj. Serikali ya kijiji cha Mwanga,iliweza kumkamata akiwa amebakiza shilingi 5,000 tu.

Ushuhuda mwingine uliotolewa kwenye mkutano huo,ni kwamba   yupo mwanaume mwingine aliweza kuchinja mbuzi (bila kibali cha familia) aliyenunuliwa na mke wake kwa fedha za TASAF, na kisha  kuuza nyama na fedha zake kuzitumia kunywea pombe.


Imedaiwa kuwa mwanamke alinunua Mbuzi huyo ikiwa ni mwanzo wa kununua Mbuzi zaidi kwa kutumia fedha za TASAF ,ili kaya yao iwe na ufugaji wa mbuzi kwa ajili ya kuipatia familia hiyo kipato cha kuwawezesha kuishi maisha bora.

Akizungumza kwenye mkutano huo,mwenyekiti wa kijiji cha Mwanga,Jackson mkoma,alisema ushuhuda huo ni sehemu tu ya vitendo vinavyofanywa na hasa na  baadhi ya wanaume vyenye lengo la kukwamisha juhudi za serikali kupitia TASAF, kuzijengea uwezo wa kiuchumi kaya maskini sana.

“Mimi na ofisi yangu kuanzia sasa tutazifuatilia kwa karibu kaya zote zinazopokea ruzuku hizi, ili tujiridhishe na matumizi ya fedha husika.Tuna uhakika kama fedha hizi zitatumika kama inavyokusudiwa,kaya husika katika muda mfupi ujao,zitaishi maisha bora.

Mkutano huo kwa pamoja umeazimia kuwa kuanzia sasa fedha za TASAF,ziwe kwenye mikono ya wanawake kwa madai kwamba ndio wenye sifa nzuri ya utunzajia wa mali ikiwemo fedha za TASAF.Pia wanao sifa ya kutumia fedha hizo kwa malengo yalioainishwa na TASAF  ambayo baadhi ni kuongeza kipato cha familia,kugharamia masomo kwa watoto wa kaya maskini na kulipia ada ya mfuko wa afya ya jamii (CHF).

Pamoja na changamoto hizo na nyingine nyingi,walengwa hao walitumia fursa hiyo kuipongeza serikali kupitia TASAF,kuwa ruzuku ya fedha hizo ambazo  zimewasaidia mno kuboresha hali zao za kiuchumi,uhakika wa chakula na matibabu tofauti na ilivyokuwa kabla ya ruzuku hizo hazijaanza kutolewa.

Aidha,wameishauri TASAF kuangalia uwezekano wa kuongeza kiwango cha ruzuku ya fedha kitakachokidhi mahitaji halisi kwa kipindi hiki.


Kwa upande wake mratibu wa TASAF wilaya ya Mkalama, Athumani Jumanne Dulle,pamoja na mafanikio makubwa ya mradi huo,kumekuwepo na matukio ya kugombea na kupigana yanayohusisha fedha za TASAF.

No comments:

Post a Comment