Monday, July 6, 2015

Makala ya madhara yatokanayo na matumizi ya Tumbaku.

Ni Tumbaku ambayo imeshakaguliwa na wataalamu wa kilimo kutoka Bodi ya Tumbaku Tanzania ikikaguliwa na mgeni rasmi wakati wa ufunguzi wa soko la Tumbaku kwa kuanza kununuliwa na makampuni yanayonunua zao hilo.

TUMBAKU ni zao pekee lenye madhara mengi ya kiafya kwa wakulima na wateja wake ambao nusu yao hupoteza maisha duniani kila baada ya sekunde nane,ambapo mtu hufariki kutokana na matumizi ya tumbaku.

Watu wanaotumia tumbaku katika umri mdogo vile vile hufariki mapema sana kabla ya kufikia umri wa miaka 25 na kwamba matumizi hayo ya tumbaku husababisha vifo milioni sita duniani kila mwaka.

Kwa mujibu wa taarifa za wataalamu wa magonjwa yatokanayo ya tumbaku nusu ya vifo vitokanavyo na uvutaji wa sigara ni kwa watu wenye umri wa kati ya miaka 30 hadi 69

Aidha uvutaji wa sigara duniani kote unachangia asilimia 12 ya vifo vyote katika nchi zinazoendelea,na kwamba wanaume ndiyo wanaokufa zaidi kutokana na uvutaji wa sigara.

Idadi kamili ya wavutaji wa sigara Tanzania haijulikani lakini ni ukweli usiopingika kwamba watu wanaoishi kwenye maeneo ya vijijini wanavuta zaidi kuliko waishio kwenye maeneo ya mijini.

ATHARI ZA TUMBAKU KIAFYA:

Athari zinazotokana na matumizi hayo ya tumbaku kiafya ni pamoja na ugonjwa wa
saratani ya mapafu na mdomo,magonjwa ya moyo,kiharusi,shinikizo la damu,kukosa mchumba au kuvunjika kwa ndoa,mwanamke mjamzito anayevuta hujifungua mtoto mfu au mwenye uzito pungufu (LBW<2.5kg).

KEMIKALI ZA HATARI KWENYE MOSHI WA SIGARA:

Moshi wa sigara una kemikali zaidi ya 4,000 na kati ya hizo,kemikali 60 huleta saratani,ambazo ni pamoja na saratani ya kemikali ya kuondoa rangi,sumu ya mchwa,Butane –gas inayotumika kwenye viberiti,kemikali iliyoko kwenye betri za magari,DDT –inayouwa wadudu kama vile mbu,Formaldehyde-inayohifadhia maiti.

MATUMIZI YA TUMBAKU BARANI AFRIKA:

Asilimia 6 -36 ya watu wazima,kila kijana mmoja kati ya kumi,huvuta tumbaku,kijana mmoja kati ya kumi hutumia vitu vitokanavyo na tumbaku.

Aidha wavulana wengi hususani asilimia 15.5 huvuta sigara kuliko wasichana ambao ni asilimia 5.2 ndiyo wanaovuta sigara,huku nusu ya vijana huvuta tumbaku bila kufahamu (remotely).

Kila sigara moja inayovutwa hupunguza maisha ya mvutaji na anayemzunguka,na upo ushahidi kwamba hasara zinazotokana na matumizi ya tumbaku ni kubwa kuliko faida zake kiuchumi na kiuchumi tumbaku itafutiwe zao mbadala.

Mwaka 1990 dunia nzima ilizalisha tumbaku tani milioni saba na baada ya kufanya mahesabu ya faida kwa mkulima,msindikaji,muuzaji,mapato kwa njia ya kodi,halafu yakilinganishwa na hasara za kuharibu misitu,gharama za tiba,kushindwa kufanya kazi kwa sababu za maradhi yanayohusishwa na sigara,kufa kabla ya wakati n.k.

WANAUME NA NGUVU ZA KIUME:

Wanaume wengi walioacha kuvuta sigara wameacha siyo kwa kuogopa magonjwa ya moyo na saratani,bali kilichowashituwa ni kuelezwa kuwa sigara hupunguza nguvu za kiume-hapo ndipo palipoleta usikivu wa kuacha sigara.

“Smoking reduces blood and causea impotence”onyo kama hilo likiwekwa kwenye paketi za sigara Tanzania litapunguza idadi ya wavutaji.

Kwa kuyatambua madhara hayo pamoja na mengine mengi,ndipo Mkuu wa Mkoa wa Singida,Dk.Parseko Kone amekuwa akisisitiza wataalamu wa kilimo kutohamasiaha zao la tumbaku kulimwa katika Mkoa huo,kati ya mazao ya biashara yaliyopewa kipaumbele.

Pamoja na madhara hayo kuwepo kwa watumiaji wa tumbaku,lakini bado wakulima wa wilaya ya Manyoni wanaendeleza kilimo cha zao hilo mwaka hadi mwaka.

Wakulima wa zao la tumbaku wa Chama Kikuu cha Wakulima kanda ya kati (CETCU) Mkoa wa tumbaku Manyoni walifanya sherehe za ufunguzi wa masoko ya ununuzi tumbaku kwa mwaka 2014/2015 kwenye Chama cha msingi cha ushirika Msemembo,wilayani Manyoni,Mkoani Singida,na kuhudhuriwa na idadi ndogo ya wakulima wa zao hilo,licha ya kuwepo vikundi vya ngoma vya kabila la wasukuma,vilivyowaburudisha wananchi,wakulima,wanachama wa vyama vya ushirika pamoja na viongozi mbalimbali wa chama na serikali.

Katika sherehe hizo mambo mbalimbali yalizungumziwa ikiwemo changamoto zilizo nje ya uwezo wa chama,ambazo ni pamoja na kampeni ya kimataifa ya kupinga uvutaji wa sigara,hali ya hewa ya ukame inayolikabili eneo la kilimo cha zao la tumbaku mara kwa mara na kutokuwepo kwa sheria ya kumbana mchoma mkaa kushiriki katika zoezi la upandaji miti.

Changamoto zilizo ndani ya uwezo wa chama ni pamoja na tabia ya kutorosha tumbaku bado inaendelea miongoni mwa baadhi ya wanachama.Utoroshaji huo unachangia kwa kiwango fulani uzoroteshaji wa urejeshaji deni la baadhi ya wakulima wasio waaminifu.


Katika Makala hii Mwenyekiti wa CETCU LTD,Bwana Florence Mpanda katika risala ya wakulima wa tumbakau wa Chama kikuu cha wakulima Kanda ya kati kwa mgeni rasmi,Mkuu wa wilaya ya Manyoni,Bi Fatuma Hassani Toufiq kwenye sherehe za ufunguzi wa masoko ya tumbaku zilizofanyika katika Chama cha Msingi cha Ushirika Msemembo anazungumzia hali ya uzalishaji wa tumbaku,taarifa ya uzalishaji kuanzia msimu wa 2010/2011 hadi 2013/2014 pamoja na mchango wa maendeleo ya kilimo cha tumbaku kwa wakulima wa tumbakau katika eneo hilo.


Marobota ya Tumbaku ya wakulima yanayosubiri kukaguliwa kabla ya soko la kununua Tumbaku halijaanza.

HALI YA UZALISHAJI WA TUMBAKU:

Anasema lengo la chama kikuu ni kuongeza uzalishaji wenye kuwezesha wanachama kupata kilo nyingi kutoka kwenye eneo dogo.Kwa mfano uzalishaji wa hekta moja uwe kilo 1,800 badala ya wastani wa kilo mia nane kwa hekta ilivyo sasa.

Anafafanua ili kutimiza azma hiyo,elimu kwa wakulima inaendelea kutolewa juu ya ujengaji wa mabani ya kisasa.Inatarajiwa kuwa baada ya misimu minne ijayo,mabani yote yatakuwa ya kisasa.

“Pembejeo zinazotumika ni zile ambazo huwa zimefanyiwa uhakiki kila mwaka na kamati ya ufundi yenye wajumbe kutoka makampuni,wanunuzi,watoa fedha,wakulima,msimamizi wa zao la tumbaku kwa niaba ya wakulima na kuongeza kwamba kwa ujumla mbali na lengo la kuongeza uzalishaji pia uzalishaji huzingatia mahitaji ya wanunuzi”alifafanua mwenyekiti huyo wa Cetcu.

TAARIFA YA UZALISHAJI KUANZIA 2010/2011 HADI 2013/2014:

“Ndugu mgeni rasmi,kuanzia 2010/2011 uzalishaji umekuwa ukishuka msimu wa 2013/2014 chama kikuu kilifanikiwa kupata kilo za tumbaku 894,939 ambazo zilikuwa na thamani ya dola za marekani 1,885,217 tu katika maeneo yanayolima tumbaku wilayani Manyoni ”anasema mwenyekiti huyo wa Cetcu Ltd.

Aidha Bwana Mpanda anafafanua kuwa katika kipindi cha masoko ya msimu wa 2013/2014,vyama vingi vilifanikiwa kuuza juu ya bei ya wastani wa taifa wa dola 2.11 kwa kilo isipokuwa vyama vya ushirika vya msingi vya Mgandu,Kintanula,Mitundu,Hika pamoja na Kalangali.

Anasema Chama cha ushirika cha msingi Makale kiliongoza kwa kuuza kwa wastani wa bei ya juu wa dola 2.32 na chama cha ushirika cha Msingi Msemembo kwa msimu wa 2012/2013 kiliongoza kwa kuuza kwa wastani wa dola 2.44.

Kwa mujibu wa mwenyekiti huyo uzalishaji wa msimu wa 2012/2013 ulishuka kwa asilimia 56 ukilinganisha na msimu wa 2011/2012 ambapo kilo zilizouzwa zilikuwa 2,105,000,kushuka huko kwa uzalishaji kumetokana na kushuka kwa bei ya tumbaku msimu wa 2010/2011.

Anasema hali hiyo itazidi kuwa mbaya kwa sababu Makampuni yanayonunua tumbaku kwa sasa yanatishia kushusha kilo za tumbaku mwaka hadi mwaka,kwa kigezo kuwa bei ya tumbaku katika soko la dunia ni mbaya.

Akifafanua zaidi anasema katika kipindi cha msimu wa mwaka 2010/2011 Chama kikuu hicho kilitarajia kuzalisha kilo 3,598,334 ambapo kilo 3,946,712 zilitarajiwa kununuliwa kwa thamani ya doka za marekani 5,135,613.09 sawa na wastani wa dola 1.30 kwa kilo.

Anasema mwenyekiti huyo wa Cetcu Ltd kuwa msimu wa 2011/2012 kilo zilizotarajiwa kuzalishwa ni 3,129,298 na kilo 2,102,064 zilitarajiwa kununuliwa kwa thamani ya dola 3,221,445.03 kwa wastani wa dola 1.53 kwa kilo.

Anasema msimu wa 2012/2013 kilo 1,450,000 zilitarajiwa kuzalishwa na kilo 923,340 zilitarajiwa kununuliwa kwa thamani ya dola 2,113,809.31 kwa wastani wa dola 2.29,wakati katika msimu wa 2013/2014 kilo 977,070 zilitarajiwa kuzalishwa huku kilo 894,939 zilitarajiwa kununuliwa kwa thamani ya dola za marekani 1,885,217.00 kwa wastani wa dola 2.11 kwa kilo.

Hata hivyo mwenyekiti huyo wa CETCU anasema msimu wa 2014/2015 Chama kikuu kinatarajia kuuza kilo 894,818 zenye thamani ya dola za marekani 1,843,325.08.

“Ndugu mgeni rasmi wakulima wa tumbaku huwa tuna utaratibu wa kufanya sherehe za ufunguzi wa masoko kila mwaka,utaratibu huu siyo wa kanda yetu pekee yake bali ni wa nchi nzima,kwa kila Union kufanya sherehe hizi na sherehe za kanda hutanguliwa na sherehe za kitaifa na kwa msimu huu sherehe za kitaifa zimefanyika katika kanda ya magharibi (WETCU LTD)Tabora mwezi mei,mwaka 2015”alisisitiza

Kuhusu mkutano wa tathimini ya zao,anasema sherehe za ufunguzi wa masoko hutanguliwa na mkutano wa tathimini ya tumbaku.Lengo la mkutano huo ni kupata tathimini ya zao na taratibu za masoko kwa nchi nzima.

“Washiriki hukumbushana mambo ya msingi ambayo yakitekelezwa vizuri na kwa haki wakulima watapata kipato wanachostahili,kimsingi watendaji wakifanyakazi yao vyema watapunguza malalamiko ya wakulima na kubakiwa na changamoto ndogondogo tu”anafafanua mwenyekiti.

WANACHAMA WA CETCU LDT:

Chama kikuu cha wakulima wa tumbaku kanda ya kati (CETCU LTD) kilianzishwa mwaka 2006 na mpaka sasa kina vyama vya msingi vya wakulima wa tumbaku 16.Katika msimu wa 2014/2015 vyama vitatu kati ya hivyo 16 havikuweza kulima kutokana na changamoto mbalimbali na vyama viwili kati ya vyama 13 vilivyolima havikufanya vizuri kutokana na changamoto za viongozi katika vyama hivyo.

MCHANGO WA MAENDELEO YA KILIMO CHA TUMBAKU KWA WAKULIMA WA TUMBAKU KATIKA ENEO LA MANYONI:

Anasema tumbaku ni miongoni mwa mazao ya biashara yanayolimwa kanda ya kati,hususani wilaya ya Manyoni.Pamoja na kuwa na uzalishaji mdogo ukilinganisha na maeneo mengine nchini yanayolima tumbaku,zao hilo lina wawezesha wananchi wengi katika wilaya ya Manyoni kuendesha maisha yao ya kila siku kwa kiwango cha juu ukilinganisha na maeneo yasiyolima tumbaku katika wilaya hiyo.

Anafafanua kuwa tumbaku pia huchangia sehemu kubwa ya pato la ndani ya Halmashauri ya wilaya ya Manyoni kupitia ushuru ambao huchangwa kutoka kila kilo inayouzwa kwa kupitia masoko halali.

Anasema Mpanda kuwa hivyo huchangia katika shughuli za kuendeleza Halmashauri ya Manyoni,na kwamba ili kuongeza kipato cha wakulima wa tumbaku na kipato cha Halmashauri hiyo pana kila sababu za kuweka nguvu za pamoja (Chama kikuu na uongozi wa wilaya) kwa ujumla kwa lengo la kusimamia uendelezaji wa zao.


“Ndugu mgeni rasmi,nasema hivyo zao la tumbaku lina changamoto nyingi,baadhi yake zinahitaji nguvu za dola katika kuzikabili,kwa hiyo nguvu na uongozi wa pamoja ndiyo suluhisho pekee”anasisitiza Mpanda kwa kujiamini zaidi.


Shamba la Tumbaku ambayo bado haijavunwa na mkulima tayari kwa ajili ya kwenda kuuzwa katika soko wakati msimu utakapowadia.

HALI YA UPANDAJI MITI:

Mwenyekiti huyo anasema malengo ya chama kikuu ni kuhakikisha kuwa ifikapo mwaka 2015 kila mwanachama atalima na kukausha tumbaku kwa kuni zilizotokana na miti aliyopanda mwenyewe bila kukata miti asili.Ili kutimiza lengo hilo chama kwa kushirikiana na wadau kimeweka mikakati ya upandaji miti ya pamoja (shamba la miti la pamoja na chama) na kutoa motisha ya pesa kwa wakulima watakaopanda miti,na kwamba mpaka msimu huu miti iliyopandwa na kupona imefikia miti 283,467.

Anasema kwa msimu huu upandaji miti haukufanyika kama ilivyokuwa imelengwa kutokana na ukame uliokuwa katika wilaya ya Manyoni na kwamba idadi kubwa ya miti iliyowahi kupandwa,ilikufa kutokana na ukame na miche mingi haikupandwa kutokana na wakulima kuhofia kupata hasara.

CHANGAMOTO:

“Ndugu mgeni rasmi,kilimo cha tumbaku kina changamoto nyingi sana ikiwemo changamoto zilizo nje ya uwezzo wa chama na changamoto zilizo ndani ya uwezo wa chama”anafafanua

Kwa mujibu wa mwenyekiti huyo changamoto zilizopo nje ya uwezo wao ni pamoja na kampeni ya kimataifa ya kupinga uvutaji wa sigara,hali ya hewa ya ukame inayoikabili eneo letu mara kwa mara na kutokuwepo sheria ya kumbana mchoma mkaa kushiriki katika zoezi la upandaji miti.

Aidha Mpanda anazitaja changamoto zilizo ndani ya uwezo wao kuwa ni tabia ya kutorosha tumbaku bado inaendelea miongoni mwa baadhi ya wanachama.Utoroshaji huo unachangia kwa kiwango fulani uzoroteshaji wa urejeshaji wa mikopo benki.

Anasema kuwa utoroshaji huo pia unaathiri malipo ya wakulima waaminifu,utoroshaji wa tumbaku kutoka chama kimoja kwenda chama kingine ili kukwepa kurejesha deni la baadhi ya wakulima wasio waaminifu.

“Ndugu mgeni rasmi,Bodi ya Uongozi wa Chama kikuu kwa niaba ya wadau wa tumbaku inashukuru kwa kutoa AMRI HALALI ya kuzuia walanguzi na kwamba yeyote atakayekamatwa akilangua mbolea ya tumbaku achukuliwe hatua kali”alisisitiza mwenyekiti

Na kuongeza kwamba”Ombi,ndugu mgeni rasmi,amri halali uliyoitoa mwaka jana ilitusaidia sana katika kudhibiti utoroshaji wa tumbaku,hivyo tunakuomba utupe msaada huo msimu huu”anasema.

Kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Manyoni,Mkoani Singida,Bwana Supeet Roine Mseya anasema katika msimu wa 2013/2014 Halmashauri hiyo ilipokea shilingi 168,305,348.05 zilizotokana na ushuru wa ununuzi wa tumbaku na kwa msimu wa 2014/2015 vile vile shilingi 173,781,348.32 zilipokelewa kutokana na ushuru wa mauzo ya tumbaku wilayani Manyoni.

Akizungumza na wakulima wa tumbaku kwa niaba ya Mkuu wa wilaya ya Manyoni,Bi Fatma Hassani Toufiq,Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo,Bwana Moses Matonya anasema malengo ya wakulima wa tumbaku ni kuongeza uzalishaji msimu hadi msimu.

Lakini Mkuu huyo anasema kwa mujibu wa risala ya wakulima hao,inaonyesha kuna changamoto za soko la tumbaku duniani,kutokana na kubadilikabadilika kutegemea mahitaji ya watumiaji wa tumbaku duniani,hivyo yawezekana wanunuzi waliopo wakapunguza uhitaji mwaka hadi mwaka kama inavyofanyika hivi sasa.

Anasema Toufiq kwamba katika hali kama hiyo serikali lazima iangalie namna ya kufanya ili kuwe na soko pana zaidi la kupambana na changamoto hiyo.

“Aidha napenda kuwasisitiza wakulima,vyama vya ushirika vya msingi na chama kikuu kufanya mambo yafuatayo ili kukabiliana na changamoto za uzalishaji wa tumbaku”anafafanua.

Mkuu wa wilaya huyo anasema ili kukabiliana na changamoto za uzalishaji wa tumbaku ni vyema kuongeza ubora wa zao la tumbaku wa kiwango cha juu kuanzishwa kwa mfumo wa maendeleo ya zao,ambao pamoja na mambo menegine unaweza kusaidia kupunguza makali ya kushuka kwa bei pale inapotokea.

Anasema ni muhimu kuangalia namna ya kuweza kusaidia tumbaku ili kuongeza thamani kwa lengo la kupata bei nzuri.

“Nawasihi vyama vyote vikuu vya tumbaku nchini kuungana kwa pamoja ili kuwa na nguvu ya pamoja itakayosaidia kupunguza kimasoko na pia kushuka bei za pembejeo  pakiwa na usimamiizi mzuri.

“Najua kwamba kwa miaka ya karibuni kumekuwa na wimbi la matatizo ya vyama vya ushirika kushindwa kurejesha mikopo kwenye taasisi za fedha na hata kuwalipa wakulima fedha zao za mauzo ya tumbaku,hivyo hiyo siyo dalili nzuri katika kuendelea kukopesheka na kujitegemea”anafafanua Bi Toufiq.

Kadhalika Bi Toufiq anasema hali hiyo inadhoofisha utoaji,ukuaji na ustawi wa vyama vya ushirika vya msingi,wakulima na serikali.

Anasema Mkuu wa wilaya kwamba ili uwepo uwezekano wa kuondokana na hali hiyo ameshauri vyama vya ushirika vya msingi sambamba na chama kikuu kuzingatia kuwepo kwa usimamizi mzuri na imara wa mikopo inayotolewa kwa ajili ya kilimo cha tumbaku.

Anafafanua pia Bi Toufiq kuwa kuwepo usimamizi katika uzalishaji wa tumbaku wenye tija na kufikia malengo waliyojiwekea,kuchukua mikopo inayoendana na kiwango cha uzalishaji wa tumbaku,kuwadhibiti wakulima na viongozi wasio waaminifu,wanaouza mbolea nje ya vyama vyao kwa mfano pembejea na tumbaku pamoja na kuimarisha umoja wao (Chama kikuu) na wasifikirie kuuvunja kwani umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu.

Mkuu huyo anasema serikali inatambua na itaendelea kutambua kuwa ushirika ni chombo cha kuunganisha nguvu za wenye mitaji midogo ili kuwa na sauti na nguvu ya pamoja katika suala la kujikwamua kiuchumi na kwa kutambua hilo serikali itahakiki kuwa ushirika huo unaimarika ili kutoa matunda yanayokusudiwa.

Anasema kilimo cha tumbaku kinahitaji nishati ya kukaushia tumbaku hadi sasa kuni ndiyo nishati ya kukaushia tumbaku,ukweli usiopingika ni kwamba kilimo cha tumbaku kinasababisha uharibifu wa mazingira kwa kukata miti kwa ajili ya kukaushia tumbaku.

Kwa kufuata sheria na kanuni za kilimo cha tumbaku anasema Bi Toufiq kwamba wakulima wanatakiwa kupanda miti 550 kwa kila mkulima anayeshiriki kilimo cha tumbaku sambamba na uoto wa asili utunzwe kwa matumizi ya baadye.

Aidha anasema vyama vya msingi vya ushirika na chama kikuu wawe na mashamba ya miti kama kielelezo katika suala la kutunza mazingira,jambo ambalo ni muhimu sana.

Kuhusu amri halali aliyotoa mwaka jana,mkuu wa wilaya huyo anasema anatambua kwamba msimu uliopita alitoa amri halali iliyokuwa ikilenga kudhibiti wakulima ambao wana tabia ya kutorosha tumbaku na kwenda kuiuza kwenye mikoa jirani ya Tabora na Mbeya,lakini mara nyingi wale wanaofanya hivyo ni wale ambao wana deni kubwa benki.

“Kusema wakulima wa aina hiyo ni wabaya sana kwa sababu kuu zifuatazo ambazo ni pamoja na kutorosha tumbaku kunasababisha Halmashauri kukosa ushuru wake,chama kikuu kukosa ushuru wake na vyama vyao kukosa ushuru wake”anasisitiza.

Anafafanua kwamba kwa kufanya hivyo wanapunguza kipato cha maeneo waliyotakiwa kuuzia mazao yao na kwa maana nyingine malengo ya shughuli za maendeleo katika sehemu hizo tarajiwa yanaathirika.

“Kwa mantiki hiyo,naendelea kusisitiza mambo niliyoyasisitiza katika ufunguzi wa masoko ya msimu uliopita kuwa viongozi wa vyama vya msingi na serikali katika maeneo yanayolima tumbaku waone taarifa katika ofisi ya wilaya juu ya walanguzi wa tumbaku nasi tutawasaidia ili tumbaku isitoroshwe kwani tumbaku ikitoroshwa kwenda mikoa mingine ya jirani inatupotezea mapato ya wilaya yetu”anafafanua Bi Toufiq.

Aidha Mkuu wa wilaya anasema anawasihi sana wakulima wasianzishe associations,kwenye ushirika kuna faida nyingi hasa ya kukopesheka kirahisi bila ya kuweka dhamana ya mali za kudumu katika taasisi za fedha.

Anasema kwa kufanya hivyo watakuwa wanaviuwa vyama vyao na mwisho wa siku watakuwa vibarua katika mashamba  ya wachache walio na uwezo kifedha,wakulima wajifunze kuweka akiba baada ya kupata fedha za mauzo ya tumbaku na inavyoonekana wengi wakipata mauzo wanatumia fedha zote.

“Tafadhali msiongeze wake na kuendekeza sherehe,uzeni tumbaku yenu mapema,kwa kufanya hivyo mtauza tumbaku ikiwa nzito na katika hali nzuri ya ubora,kilimo cha tumbaku kinahusisha ukaushaji wa tumbaku kwa kutumia kuni,nawasihi sana pandeni miti ya kutosha kama sera ya tumbaku inavyosema ili kupunguza uharibifu wa mazingira kutokana na kukata miti asili.

Hata hivyo mkuu wa wilaya huyo katika hotuba yake hiyo anasisitiza wakulima wasitoroshe tumbaku,kwani wakifanya hivyo wataviachia vyama vyao mzigo mkubwa wa madeni na hatima yake havitakopesheka.

“Naamini kama mna wasiwasi kuwa mnaweza kukosa malipo kaeni na benki inayowakopesha kuona jinsi gani mnaweza kusaidiana”alisema


“Wakulima rudini shambani,kwenye tumbaku kuna faida nyingi mkulima wa tumbaku anakopeshwa pembejeo za tumbaku na mahindi, hivyo nawasihi tumieni fursa hii vizuri,fuateni maelekezo ya wataalamu wenu”anasisitiza Bi Toufiq.

No comments:

Post a Comment