Friday, September 16, 2011

TATIZO LA KUKOSEKANA KWA UMEME KATIKA KIWANJA CHA NDEGE CHA KIMATAIFA CHA JULIUS NYERERE USIKU WA TAREHE 10 SEPTEMBER, 2011


Usiku wa Jumamosi tarehe 10 Septemba, 2011 kulitokea hitilafu ya kiufundi ya umeme katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere hali iliyosababisha kuvurugika kwa ratiba za ndege kadhaa ambazo wakati huo zilipaswa kuruka au kutua katika kiwanja hicho


Kutokana na hitilafu hiyo baadhi ya ndege zililazimika kuahirisha safari zao kwa kushindwa kuruka na nyingine ziililazimika kutua katika viwanja vingine vya jirani kama vile Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro, Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Zanzibar na Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Jomo Kenyatta nchini Kenya.


Mamlaka ya Viwanja vya Ndege inapenda kutoa ufafanuzi wa kuhusu chanzo cha tatizo hilo na hatua zilizochukuliwa kama ifuatavyo:


Chanzo cha tatizo hilo la kiufundi ni kushindwa kufanyakazi kwa mfumo wa mitambo unaotenganisha umeme unaofuliwa na jenereta za dharula kuruhusu matumizi ya umeme wa TANESCO. Hali hii ilipelekea kiwanja kuendelea kutumia jenereta za dharula hadi tatizo hilo liliporekebishwa asubuhi ya jumapili tarehe 11/09/2011 kwa ushirikiano wa wataalam wa TAA na TANESCO.


Wakati kukiwa na tatizo hilo katika mfumo wa mitambo ya kutenganisha matumizi ya umeme kulijitokeza hitilafu nyingine ya kuzimika kwa taa katika njia ya kurukia na kutua ndege na hivyo kushindikana kwa ndege kutua au kuruka kwa kipindi chote hicho.




Kufuatia hali hiyo wahandisi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege waliweza kufanya matengenezo ya mfumo huo wa umeme na Mnamo saa 7.30 usiku wa manane wataalam hao waliweza kufanikiwa kurudisha umeme kiwanjani hapo na kufanya baadhi ya ndege kuruka na kutua. Matengenezo kamili ya mfumo huo yalikamilika siku ya Jumapili, tarehe 11 Septemba, 2011. Kwa sasa shughuli za uendeshaji kiwanjani hapo zimeendelea kama kawaida.


Kikundi kazi cha wataalam kimeshaundwa kufanyia kazi suala hilo kwa undani zaidi kwa lengo la kupata kiini cha tatizo hilo, kufanya tahmini ya athari ziliopatikana na pia kutafuta ufumbuzi wa kudumu wa tatizo hilo kwa lengo la kuhakikisha kwamba halijitokezi tena.


Mamlaka ya viwanja vya ndege Tanzania inasikitika sana kwa usumbufu na hasara zilitokana na tatizo hilo na tunawaomba radhi wateja wetu wote , hususani mashirika ya ndege, abiria, wadau wote na wananchi kwa ujumla.


Mwisho tunapenda kuwahakikishia kuwa hitilafu hiyo ya umeme ambayo kwa bahati mbaya ilitokea kiwanjani hapo usiku huo wa kuamkia tarehe 11 Septemba, 2011 halina uhusiano wowote na tishio la kigaidi kama ambavyo baadhi ya watu walihusisha tatizo hilo na lile lililotokea nchini Marekani tarehe 11 Septemba, 2001. Tunawahakikishieni kuwa kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere kina ulinzi wa kutosha kuthibiti matukio kama hayo ya kigaidi.


Mhandisi. Suleiman S. Suleiman


KAIMU MKURUGENZI MKUU

No comments:

Post a Comment