Monday, June 24, 2013

Mwanafunzi wa kike mkoani Singida adaiwa kutelekeza mtoto wa miezi mitano.

Mkuu wa wilaya ya Singida, mwalimu Queen Mlozi akiwa amempakatia mtoto wa kiume ambaye inadaiwa kutelekezwa kwenye pagara la nyumba na mama yake ambaye anasoma chuo cha uhasibu tawi la Singida.Mtoto huyo mwenye umri wa miezi mitano, amehifadhiwa wodi sita (b) katika hospitali ya mkoa mjini Singida.
Mwanafunzi wa kike wa chuo cha uhasibu tawi la mkoa wa Singida ambaye
hajafahamika jina lake, amemtelekeza mtoto wake wa kiume mwenye umri wa miezi mitano ndani ya jengo la nyumba (pagala) ambayo bado haijamalizika kujengwa.
Mkuu wa wilaya ya Singida Mwalimu Queen Mlozi, amesema mwanafunzi huyo ametenda unyama huo usiku katika kijiji cha Misake nje kidogo ya Singida mjini.
Amesema motto huyo mwenye afya njema kabisa, ameokotwa na raia wema baada ya kusikia akilia ndani ya pagala la nyumba.
Mlozi amesema kwa mujibu wa raia hao wema, walikuta mtoto huyo akiwa ametandikiwa shuka vizuri na kufunikwa kwa blakenti ndogo.
Mkuu huyo wa wilaya amesema jeshi la polisi limechukua kadi ya kliniki iliyotolewa na zahanati ya Mandewa ili kufuatilia jina la mama na baba wa mtoto huyo.
Amesema taarifa zilizopatikana eneo la tukio, zanadai kuwepo kwa mwanafunzi wa uhasibu aliyekuwa akiishi na mtoto kwenye hosteli na baada ya tukio mwanafunzi huyo ametoweka.

1 comment:

  1. Jamani, mbona inauma sana? Mtoto ameshaishi miezi mitano, kwa nini asingemwombea hata ustawi wa jamii? Au angejieleza kwa ndugu zake akasaidiwa? Hata kama amepata matatizo gani, si haki kumtelekeza mtoto hivyo.

    ReplyDelete