Wednesday, March 12, 2014

Hospitali ya Rufaa Singida yakabiliwa na uhaba wa watumishi wa afya.


Sehemu ya Majeengo ya Hospitali ya Rufaa mkoani Singida inayokabiliwa na uhaba wa Watumishi wa Afya.

HOSPITALI ya Rufaa mkoani Singida,inakabiliwa na uhaba wa watumishi zaidi ya mia mbili wa kada mbalimbali,kitendo kinachochangia huduma kutokukidhi mahitaji.

 Hospitali hiyo ambayo ipo nje ya mji wa Singida katika barabara ya Sepuka,kwa sasa imeanza kutoa huduma kwa wagonjwa wa nje.Huduma zingine ikiwemo ya akina mama kujifungua,bado hazijaanza.

Hayo yamesemwa na Afisa Muuguzi wa hospitali hiyo, Pendaeli Masai wakati akitoa taarifa yake kwa mkuu wa mkoa wa Singida, Dk.Parseko Kone aliyetembelea hospitali hiyo kujua maendeleo yake.

Amesema  kuwa licha ya hospitali hiyo kuwa  na vifaa   vya kisasa,huduma mbalimbali hazijaanza kutolewa kutokana na uhaba mkubwa wa watumishi.        

 “Tumeanza kutoa huduma kwa wagonjwa wa nje Desemba mwaka jana na kwa kuanzia tumeanza na watumishi
40 wa kanda mbalimbali.Hawa watumishi hawatoshi,hali inayopelekea tushindwe kutoa huduma zingine ikiwemo ya akina mama kujifungulia”,amesema Pendaeli.

Kwa upande wake mkuu wa mkoa wa Singida.Dk.Parseko Kone,baada ya kukagua hospitali hiyo,amesema majengo mawili ndiyo yaliyokamilika na mengine saba yanaendelea kujengwa.

Dk.Kone amesema yatakapokamilika majengo hayo, inatarajiwa hospitali hiyo itakuwa na uwezo wa kuhudumia mikoa ya Singida, Tabora, Simiyu, Dodoma, Shinyanga na Manyara.


Naye kaimu mganga mkuu mkoa wa Singida, Dk.Musa Kimala amesema kuwa zaidi ya shilingi milioni 400 zimetumika kununulia vifaa mbalimbali ikiwemo vitandavya upasuaji,mashine za hewa.

No comments:

Post a Comment