Saturday, August 31, 2013

Makundi ya watu tofauti mkoani Singida wapendekeza Tanzania kuwa na muundo wa serikali tatu.

 Mjumbe wa baraza la Katiba kwa watu wa makundi mbalimbali mkoani Singida Mussa Sima akitoa maoni ya kikundi chao juu ya uboreshaji wa rasimu ya Katiba katika kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa chuo cha wananchi mjini Singida.
 Baadhi ya viongozi wa mashirika yasiyo ya kiserikali ya mkoa wa Singida wakishiriki kikao cha rasimu ya katiba katika kikao kilichofanyika kwenye ukumbi wa mikutano cha chuo cha maendeleo ya wananchi mjini Singida.
Baadhi ya wajumbe wa baraza la rasimu ya Katiba kutoka kwenye makundi mbalimbali, wakiwa kwenye kikundi kujadili uboreshaji wa rasimu ya katiba.

Baadhi ya wajumbe wa baraza la rasimu ya katiba kwa watu kutoka makundi mbalimbali katika manispaa ya Singida, wamependekeza kuundwa kwa muungano wa serikali tatu na kudai kila serikali inufaike na raslimali zake.

Wakifafanua, wamependekeza muungano huo uwe na serikali ya muungano wa Tanzania, serikali ya Tanzania bara na serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Wamesema kila serikali inufaike peke yake na
rasilimali zake, pia kila serikali itambulike na umoja wa mataifa na uwepo usawa wa madaraka katika muungano.

Mambo yaliyopendekezwa kuwepo kwenye muungano ni jeshi/ulinzi, usalama, muundo wa mahakama, bunge na bendera ya muungano.

Aidha, wajumbe wengine wamependekeza katiba ijayo iendelee kutambua serikali mbili zilizopo za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Wajumbe hao wamedai kuwa serikali tatu haitakuwa na nguvu ya kujiendesha na mbaya zaidi itategemea mikopo kutoka ndani na nje ya Jamhuri ya Muungano ili iweze kujiendesha.

Itakuwa mzigo mzito kwa wananchi kwa vile watakamuliwa zaidi katika kutozwa kodi.

Mambo ambayo wamependekeza yawemo kwenye muungano wa serikali mbili, ni pamoja na elimu,mahakama,mawasiliano (posta,simu,anga na bandari).

Pia wajumbe wengine wamependekeza katiba ijayo iwe na serikali moja kwa madai kwamba itakuwa na nguvu zaidi.

Wakiijengea nguvu hoja yao hiyo, wamesema serikali moja,itaipinguzia serikali ya sasa ukubwa wa majukumu yake na itatoa ushindani wa maendeleo kimajimbo.


Aidha, wamependekeza wabunge wabaki kuwa wabunge na wasipewe majukumu menginei kama ya uwaziri,ili waweze kuwajibika ipasavyo kwa wananchi waliowapigia kura.

No comments:

Post a Comment