Friday, February 15, 2013

SAMMAYUNI WA SINGIDA AONESHA UKATILI ULIOKITHIRI

Jeraha la Mwanamke (30) aliyeunguzwa pasi ya umeme na mumewe mjini Singida.

Jeshi la polisi Mkoani Singida linamshikilia mtu mmoja Baltazar Mushi Sammayuni (33), kwa tuhuma ya kumuunguza mkewe usoni, kwa kutumia pasi ya umeme wakati akiwa amelala usiku wa manane nyumbani kwao.
Kaimu kamanda wa polisi mkoani Singida Thobias Sedoyeka amesema tukio hilo la kusikitisha lilitokea siku ya
ijumaa iliyopita saa kumi alfajiri nyumbani kwao katika eneo la Ipembe mjini Singida.
Amesema kuwa, Sammayuni anayejishughulisha na biashara, alifunguliwa mlango usiku, lakini kutokana na sababu ambazo bado zinachunguzwa aliiwasha pasi ya umeme wakati mkewe akiwa kwenye usingizi mzito na kumuunguza usoni sehemu ya shavu la kushoto.
Amesema kuwa mwanamke huyo amejeruhiwa vibaya lakini baada ya kupatiwa tiba katika hospitali ya mkoa wa Singida aliruhusiwa na hali yake inaendelea vema.
Sedoyeka amesema kuwa wanatarajia kumfikisha mtuhumiwa mahakamani wakati wowote  baada ya upelelezi kukamilika.
Kutokana na tukio hilo, Sedoyeka ametoa wito kwa wanandoa kuacha kujichukulia sheria mkononi kwa kuwa kila mtu anayo haki ya kuishi na yeyote atakayekiuka, mkono wa sheria utafanya kazi yake.
Aidha mwanamke huyo (30) akizungumza na Singida Yetu Blog nyumbani kwake mjini Singida kwa sharti la kutotajwa jina, amesema baada ya mumewe kufika usiku na kumfungulia mlango, yeye alilala lakini alishitushwa na maumivu makali usoni hali iliyomlazimu kuamka ghafla.
Amesema alikimbilia kwenye kioo kikubwa na alipojitazama aligundua uso wake sehemu ya shavu la kulia ameunguzwa na pasi na alipomuuliza mumewe sababu ya kuchukua uamuzi huo alijibiwa kuwa ameamua tu kufanya hivyo.
“Kwa kweli roho inaniuma sana, nilipomuuliza akanijibu ameamua tu kufanya hivyo?…kesho yake akanieleza kumbe hata jicho sikutoboa”, nilitakiwa na hayo macho yote niyatoboe kabisa ili usiendelee kuona tena,”alisema mwanamke huyo jinsi mumewe alivyomkejeli.
Sedoyoka ambaye ni mkuu wa upelelezi makosa ya jinai amesema mtuhumiwa atafikishwa mahakamani wakati wowote wiki hii kujibu shitaka lake.

No comments:

Post a Comment