Saturday, April 26, 2014

Halmashauri Mkoa na Manispaa Singida zadaiwa zaidi shilingi 6.3 bilioni na wakandarasi.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mh. Mizengo Pinda.

SEKRETARIETI ya Mkoa na Halmashauri za wilaya na manispaa mkoani Singida zinadaiwa na wakandarasi,wazabuni na watumishi wa umma zaidi ya shilingi 6.3 bilioni hadi novemba mwaka jana.

Madeni hayo yameainishwa kwenye taarifa ya madeni ya mkoa wa Singida iliyotolewa mbele ya kikao cha kamati ya ushauri wa mkoa (RCC) kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa chuo cha VETA mjini Singida.

Taarifa hiyo imedai kwamba halmashauri za wilaya na manispaa,zinadaiwa zaidi ya shilingi 2.4 bilioni na wakandarasi,wakati wazabuni wanadai zaidi ya shilingi 314.9 milioni.

Kwa upande wa sekretariati ya mkoa,inadaiwa na wakandarasi zaidi ya shilingi milioni tisa na wazabuni shilingi 526.6 milioni.

Kwa upande wa madeni ya walimu na watumishi wasio walimu,halmashauri zinadaiwa zaidi ya shilingi 2.7 bilioni zikiwa ni madeni ya walimu na zaidi ya shilingi 1.3 bilioni na watumishi wasio walimu.

Sekretarieti ya mkoa inadaiwa na walimu zaidi ya shilingi 525.6 milioni na zaidi ya shilingi 120.7 milioni na watumishi wasio walimu.

Aidha, taarifa hiyo imetaja athari zinazosababishwa na madeni hayo makubwa,ni serikali kutoaminika na
miradi kuongezeka gharama kutokana na mfumuko wa bei.

Athari zingine ni pamoja na serikali kutozwa riba kwa fedha zilizocheleweshwa kulipwa baada ya kazi kufanyika,watumishi kukosa morali au hamasa ya kufanya kazi na kukosekana kwa huduma muhimu kama umeme mashuleni,maji na vyakula.

No comments:

Post a Comment