Monday, May 19, 2014

Elekezeni nguvu zenu kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa – Tindu Lissu.

Mbunge Tundu Lissu, Singida Mashariki

MBUNGE wa Jimbo la Singida mashariki kupitia tiketi ya CHADEMA, Tundu Lissu amewataka wananchama wa chama hicho kata ya Iseke tarafa ya Ihanja wasibweteke na ushindi wa udiwani walioupata katikati ya mwaka jana, na badala yake waelekeze nguvu zao zote kwenye uchanguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika oktoba mwaka huu.

Amesema ushindi huo utakuwa na maana zaidi endapo CHADEMA itazoa nafasi zote za uenyeviti wa vitongoji na vijiji katika wilaya yote ya Ikungi, mkoa wa Singida.

Tundu alitoa wito huo hivi karibuni wakati akizungumza kwenye hafla ya kupongezana kwa ushindi wa nafasi ya udiwani wa kata ya Iseke, uliopatikana Juni mwaka jana kwenye uchaguzi mdogo.Hafla hiyo iliyofana ilifanyika kwenye bwalo la shule ya sekondari Iseke.

Amesema Halmashauri ya wilaya ya Ikungi,ina madiwani 35 kati yao wa CHADEMA ni watatu tu idadi ambayo inachangia kutokuwepo na uwiano mzuri katika kutoa mchango kwenye vikao vya maamuzi.

“Kwa hali hii ukiangalia idadi hiyo utabaini kwamba bado kazi kubwa ipo mbele ya CHADEMA ya kuhakikisha inakuwa na idadi inayoshabiriana na ya CCM au kuwa na idadi kubwa zaidi ya CCM lengo hasa iwe ni kuwa na idadi kubwa zaidi ya CCM”,alifafanua Mbunge huyo.

Aidha,Tundu amesema ushindi walioupata wana CHADEMA Iseke ni ukombozi mkubwa kwao kwa sababu
watakuwa hawasumbuliwi tena kuchangia mali na nguvu zao katika maendeleo yao kwenye sekta mbalimbali.

“Suala la kuiletea maendeleo kata hii ya Iseke ni jukumu la serikali pekee na wala sio la wananchi nasema hivyo kwa sababu serikali ina fedha za kutosha kutekeleza miradi yote ya wananchi”,amesema.

Nafasi ya udiwani ya kata ya Iseke tarafa ya Ihanja wilaya ya Ikungi ilikuwa wazi baada ya aliyekuwa diwani kupitia tiketi ya CHADEMA Amosi kuhama CHADEMA na kurejea CCM Amosi aliomba nafasi hiyo kupitia CCM lakini aligarangazwa na Emmanuel Jingu wa CHADEMA.

No comments:

Post a Comment