Tuesday, September 17, 2013

Wafanyakazi wa Wakala Jiolojia wajeruhiwa wakidhaniwa ni Majambazi na wanyonyaji Damu

 Mfanyakazi wa muda wa wakala waJiolojia mkoani Dodoma na mwanafunzi wa mwaka wa pili katika chuo kikuu Dodoma anayesomea masomo ya Jiolojia, Edwin Rwekiza (25) akipatiwa matibabu katika hospitali ya mkoa baada ya kupigwa vibaya na baadhi ya wananchi wa kijiji cha Irisya wilaya ya Ikungi kwa kuhisiwa kuwa ni Jambazi na mnyonya damu za Binadamu. Edwin amesafirishwa kupelekwa hospitali ya KCMC Moshi mkoani Kilimanjaro kwa matibabu zaidi.
 Mfanyakazi wa wakala wa Jiolojia  Dodoma mjini,Peter Lucas akiwa katika hospitali ya mkoa mjini Singida kutibiwa majeraha yaliyotokana na kupigwa vibaya na wananchi wa kijiji cha Irisya. Wananchi hao pamoja na kuonyeshwa vitambulisho na wafanyakazi hao,hawakuwaamini na kuendelea na imani yao kuwa ni Majambazi na wanyonya Damu za Binadamu.
 Mganga wa zamu katika hospitali ya mkoa, Dk.Reginald Pweleza akizungumzia hali za majeruhi (wafanyakazi wa wakala wa Jiolojia kutoka Dodoma) waliopigwa na wananchi wa kijiji cha Irisya baada ya kuwahisi kuwa ni majambazi na wanyonya Damu za Binadamu.
 Kamishna msaidizi wa madini kanda ya kati Singida,Manase Mbasha,akitoa taarifa kwa waandishi wa habari (hawapo kwenye picha) juu ya wafanyakazi wa wakala wa Jiolojia  kutoka Dodoma,kupigwa na wananchi wa kijiji cha Irisya wilaya ya Ikungi.
    Jengo la ofisi ya madini mkoani Singida.
WAFANYAKAZI wawili wa Wakala wa Jiolojia kutoka Dodoma mjini,wamepigwa na kujeruhiwa vibaya wakiwa kazini na baadhi ya wananchi wa kijiji cha Irisya tarafa ya Sepuka wilaya ya Ikungi,kwa madai ya kuhisiwa kuwa ni majambazi na wanyonyaji damu.

Wananchi hao waliwavamia Peter Lucas (30) na Edwin Rwekiza (25), wakiwa kazini na kuwapiga kwa kutumia silaha za jadi ikiwemo marungu.

Wafanyakazi hao wameumizwa vibaya vichwani na Edwin ambaye ni mwanafunzi wa Chuo Kikuu Dodoma mwaka wa pili akichukua masomo ya Jiolojia,amevunjika mifupa ya kichwani na hali yake ni mbaya.

Juzi jioni Edwin amesafirishwa kwa ndege kupelekwa hospitali ya KCMC Moshi mkoani Kilimanjaro,kwa matibabu zaidi.Kwa upande wake Peter,yeye anaendelea na matibabu katika hospitali ya mkoa mjini hapa.

Wakala huo ambao unafanya kazi chini ya Wizara ya Madini na Nishati,wafanyakazi wake hao wako mkoani Singida kwa kazi ya kuchora ramani za kijolojia.

Shughuli zingine ni uchunguzi kwa kutumia kemikali,ili kubaini madini na kwa ujumla walikuwa
wakifuatilia uchunguzi wa madini mkoani Singida,uliofanywa kwa njia ya matumizi ya helkopta miezi michache iliyopita.

Akizungumza na Singida Yetu ofisini kwake juzi,Kamishina Msaidizi wa Madini kanda ya kati Singida,Manase Mbasha,alikiri kutokea kwa tukio hilo na kwamba limetokea septemba 11 mwaka huu majira ya jioni huko katika kijiji cha Irisya.

Alisema Ofisi ya Mkuu wa Mkoa imewaandikia wakuu wa wilaya zote juu ya ujio wa wafanyakazi wa wakala wa jolojia kutoka Dodoma, kufanya kazi katika maeneo yaliyobainishwa kuwa na dalili ya madini kupitia uchunguzi uliofanywa kwa helkopta.

“Kama hiyo haitoshi,ofisi yangu nayo tuliwapa watumishi wa wakala huo, barua za kuwatambulisha katika maeneo wanayotakiwa kufanyia kazi.Cha ajabu wananchi wa kijiji cha Irisya pamoja na kuonyeshwa barua zote hizo na vitambulisho vya wafanyakazi hao,hawakuwaamini na badala yake wakajichukulia sheria mkononi”,alisema Mbasha kwa masikitiko.

Alisema pamoja na wafanyakazi hao kujeruhiwa vibaya,pia gari la serikali walilokuwa wakilitumia STK.8756 vyoo vyake vyote,vimevunjwa kwa kupigwa mawe na rungu.

“Natoa wito kwa wananchi wa mkoa wa Singidas,kurejesha utamaduni wao uliozoeleka wa kufuata taratibu,kanuni na sheria pale wanapokuwa na wasi wasi na wageni wanaoingia katika maeneo yao.Waache kufuata utamaduni wanaopandikizwa”,alisema.

No comments:

Post a Comment