Monday, February 24, 2014

Mifuko ya Bima ya Afya (NHIF) na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) Singida yahimizwa kuwa makini kwa madai ya kughushi.

Meneja wa NHIF mkoa wa Singida, Agnes Chaki, akifungua kikao cha waratibu wa mfuko wa Taifa Bima ya Afya na wale wa mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) ambacho kilitumika kukumbushana juu ya utoaji huduma bora kwa wananchama.Kulia ni afisa matekelezo na uratibu NHIF mkoa wa Singida,Isaya Shekifu na kushoto ni Edwin Mwangajilo afisa udhibiti ubora NHIF.
Afisa matekelezo na uratibu wa mfuko wa taifa wa Bima ya Afya (NHIF)  mkoa wa Singida, Isaya Shekifu akitoa mada yake kwenye kikao cha wataribu wa mfuko wa NHIF na mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) mkoa wa Singida.Kikoa hicho kililenga kubadilishana uzoefu juu ya utendaji kazi,ili kuboresha zaidi huduma za mifuko hiyo.Kushoto ni meneja wa NHIF mkoa wa Singida, Agnes Chaki.
Afisa udhibiti ubora NHIF mkoa wa Singida, Edwin Mwangajilo,akitoa mada yake kwenye kikao cha waratibu wa NHIF na CHF kilichofanyika  kwenye ukumbi mdogo wa mikutano wa kanisa katoliki mjini Singida.Kushoto ni meneja NHIF mkoa wa Singida, Agnes Chaki.
Baadhi ya waratibu wa mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya na wale wa mfuko wa Afya ya Jamii mkoa wa Singida, waliohudhuria kikao cha kubadilishana uzoefu katika utendaji kazi, ili kuboresha huduma zaidi.
WARATIBU wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) mkoani Singida,wamehimiza kuwa makini zaidi kukabiliana na wimbi la madai ya kughushi, kwa madai kwamba vitendo hivyo,vitachangia kudhoofisha huduma zinazotolewa na mifuko hiyo.

Wito huo umetolewa na meneja wa NHIF mkoa wa Singida,Agnes Chaki,wakati akizungumza kwenye ufunguzi wa kikao cha waratibu wa NHIF na CHF mkoani hapa, kilichofanyika kwenye ukumbi mdogo wa mikutano wa kanisa katoliki mjini hapa.

Alisema kuna baadhi ya watoa huduma si waaminifu  na wanaleta madai ya kugushi, na mfuko umejiandaa kikamilifu kuhakikisha unadhibiti vitendo hivi ili kutimiza lengo la msingi la kuwapa huduma bora wanachama wake

“Ninyi waratibu ninawaomba ndugu zangu, tusaidiane katika kupambana na hili tatizo.Mnapokutana na watoa huduma,naomba mjaribu kuwaelimisha kuwa wawe wanatibu kwa kuzingatia miongozo ya NHIF na ile ya wizara.Wahakikishe kile wanachokitoa kinakuwa ni sawa na wanacho wasilisha NHIF….mfano katika dawa”,alisema Chaki.

Aidha,meneja huyo wa mkoa, alisema mwanachama,mratibu au kiongozi ye yote akisikia au kuona  kuna vitu/vitendo vinafanyika kinyume na taratibu za NHIF,tafadhali atoe taarifa mapema ofisi za NHIF mkoani hapa,ili ziwezekufuatiliwa mapema kabla havijaleta madhara kwa mfuko.

Kwa upande wake afisa matelekezo na uratibu NHIF mkoa wa Singida,Isaya Shekifu,akitoa mada yake ya majukumu ya waratibu wa NHIF/CHF,aliwataka waratibu hao kuhakikisha
wanatimiza majukumu yao  kwa uadilifu na kwa ushirikiano baina yao ili kuongeza ufanisi na pia wanajitambulisha kikamilifu katika vituo vyao vya kazi,ili wanachama wa mifuko hiyo,waweze kuwafahamu na kuwatambua .

“Pia hakikisheni mnatatua mapema matatizo/kero zinazohusu wanachma wa NHIF/CHF pamoja na watoa huduma na muandae taarifa za utekelezaji kila baada ya miezi mitatu”,alisema Shekifu.

Afisa huyo wa maelekezo na uratibu,alisema NHIF inategemea endapo waratibu watatimiza majibu wao kwa uhakika, malalamiko kuhusu huduma za NHIF yatapungua na huduma zitaboreka.

Pia afisa udhibiti na uhakiki ubora wa NHIF mkoa wa singida ,Dr.Edwin Mwangajilo aliwasisitizia waratibu wa NHIF kuhakikishia wanapitia madai kwa uangalifu ili kuepusha makosa ambayo yanaweza kupunguza kiasi cha malipo ya madai kwa watoa huduma.

“Tunategemea mtafanya kazi zenu kwa ufanisi na uadilifu na kuhakikisha mnasimamia vituo vyote vile vya serikali,binafsi na mashirika ya dini ili wanachama wetu wa NHIF na CHF wapate huduma bora ,alifafanua Mwangajilo.

No comments:

Post a Comment