Monday, March 11, 2013

Watatu wapoteza maisha mkoani Singida katika ajali ya basi kutokana na uzembe wa dereva na mwendo kasi.

 Abiria mmoja raia wa nchini China, ambaye jina lake halikufahamika mara moja ambaye amevunjika mguu wa kushoto akipewa huduma za matibabu mara baada ya ajali ya basi la Green star lililogonga lori la mbao katika eneo la kijiji cha Isuna wilaya ya Ikungi.
 Baadhi ya majeruhi wakiwa nje ya maabara ya hospitali ya mkoa wa Singida,wakisubiri kupata matibabu.
Baadhi ya wakazi wa mji wa Singida,wakiwa nje ya maabara ya hospitali ya mkoa,kuwaona majeruhi wa ajali ya basi la Green star iliyotokea jana (10/3/2013) katika kijiji cha Isuna wilaya ya Ikungi.

Watu watatu wamefariki dunia baada ya basi T.939 BRA aina ya Yutong, lililokuwa likitokea Dar-es-salaam likielekea Kahama mkoani Shinyanga, kugonga kwa nyuma lori T.268 CCC  likivuta tela T.931 CBU aina ya Scania.
Watu hao waliofariki kwenye ajali hiyo ni
dereva wa basi hilo Yassin Ramadhani (39) na msaidizi wake (utingo) Mansory Mohamed (30).
Wafanyakazi hao wa basi hilo wamefariki wakiwa wanapatiwa matibabu kwenye maabara ya hospitali ya mkoa mjini Singida.
Mwingine aliyefariki kwenye ajali hiyo ni mtoto wa kiume anayekadiriwa kuwa na miaka mitano ambaye alifariki papo hapo kwenye eneo la tukio, hata hivyo,jina lake halikuweza kupatikana mara moja.
 Kamanda wa polisi mkoa wa Singida Linus Sinzumwa akiongea na Singida Yetu Blog alimesema ajali hiyo imetokea katika kijiji cha Nkuhi tarafa ya Ikungi wilaya ya Ikungi katika barabara kuu ya Dodoma – Mwanza.
Amesema pia katika ajali hiyo, jumla  ya abiria 20 wakiwemo raia watano kutoka China na Uganda, walijeruhiwa na wamelazwa katika hospitali ya mkoa wa mjini Singida wakipatiwa matibabu.
Sinzumwa ametaja raia kutoka China waliojeruhiwa ni Pisha Leng (45) amevunjika mguu wa kushoto, Changshing Chang (43) na Guongrung Gang na wote wanafanya kazi katika kampuni ya CCCC iliyopo Nzega mkoani Tabora.
Ametaja raia wengine kutoka Uganda kuwa ni Swahibu Semgenyi (50) amevunjika mguu wa kulia, Everine Mbine (33) na Tusime Aneti (33) na wote ni walimu kutoka chuo cha Uganda.
Amesema chanzo cha ajali hiyo ni uzembe wa dereva wa basi hilo kutaka kulipita lori lambao ambalo lilikuwa mbele.
Kamanda Sinzumwa ametumia fursa hiyo, kuwakumbusha madereva wa vyombo vya moto kujenga utamaduni wakuchukua tahadhari wakati wote ili kupunguza uwezekano wakutokea kwa ajali zinazosababisha vifo na uharibifu wa mali.

No comments:

Post a Comment