Friday, October 18, 2013

UVCCM Singida waambiwa kujiandaa na uchaguzi wa serikali za mitaa mwakani.


 Baadhi ya wananchama wa umoja wa vijana CCM (UVCCM)  wilaya ya Ikungi mkoa wa Singida wakiwa kwenye picha ya pamoja muda mfupi baada ya kumaliza kongamano la siku nne lililofanyika katika kijiji cha Mutunduru tarafa ya Sepuka jimbo la Singida Magharibi.

Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Singida, Naomi Kapambala amewaagiza wanachama wa umoja wa vijana (UVCCM) kujiandaa kikamilifu kwa ajili ya uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika mwakani.

Kapambala ametoa agizo hilo wakati akizungumza na baadhi ya wananchama wa UVCCM, Wilaya ya Ikungi waliohudhuria kongamano lililofanyika katika kijiji cha Mutunduru tarafa ya Sepuka jimbo la Singida magharibi.

Amesema vijana wakifanya maandalizi mazuri mapema kwa ajili ya uchaguzi huo,hatua hiyo itasaidia CCM kuendelea kushinda chaguzi mbalimbali kwa kishindo.

“Wapinzani wao tuendelee kuwapa fursa ya kuandamana barabarani tu,wasipewe kabisa fursa za kushinda chaguzi zo zote.Fursa za kushinda chaguzi mbalimbali ziendelee kuwa za CCM ili pamoja na mambo mengine,kiendelee kudumisha amanai na utulivu”,alifafanua Kapambala.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa UVCCM Wilaya ya Ikungi,John Mathias amesema katika
kongamano hilo lililoanza oktoba 10 – 14 mwaka huu na kuhudhuriwa na vijana 207,dhumuni lake ni kuwaweka vijana kuwa wamoja.

Aidha,Mathias alitaja baadhi za mada zilizotolewa kuwa ni pamoja na ujasiriamali,ufugaji bora wa nyuki,kuunda vikundi,kubuni miradi,andiko la mradi,uzalendo na wajibu wa vijana.

“Pia wakati wa kongamano,vijana walishiriki kazi za mikono.Tumeweza kufyetua matofali 3,502 kwa ajili ya ujenzi wa chumba cha darasa katika shule ya msingi ya Mtakuja,na tumetegeneza miziga 30″alisema mwenyekiti huyo.

Katika hatua nyingine,Mathias amesema kuwa wameweka mkakati wa kuanzisha mashamba ya vijana ya ekari 200 kwa kila jimbo la Singida mashariki na Singida magharibi.


“Kuna mwanaCCM ameonyesha nia ya kutuunga mkono katika kuanzisha mashamba haya ya vijana kwa kutupa msaada wa matrekta ya kulimia.Mashamba haya ambayo yatamilikiwa na vikundi vya vijana,kwa njia hiyo,vijana watakuwa wamejingea mazingira mazuri ya kukopesheka na taasisi za kifedha”,alisema mwenyekiti huyo.

No comments:

Post a Comment