Thursday, January 9, 2014

Wadau wa Afya Singida waridhia mpango wa Tiba kwa kadi.

Mkuu wa mkoa wa Singida, Dk.Parseko Vicent Kone akizungumza kwenye uzinduzi wa mpango wa Tiba kwa kadi (TIKA) katika halmshauri ya manispaa ya Singida uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Aque Vitae Resort mjini Singida. Kushoto ni mkuu wa wilaya ya Singida, Queen Mlozi.
 Meneja msaidizi wa mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya mkoa wa Singida, Isaya Shekifu, akizungumza muda mfupi kabla ya kumkaribisha mkuu wa mkoa wa Singida.Dk.Parseko Kone, kuzindua mfuko wa Tiba kwa kadi (TIKA) katika manispaa ya Singida. Walioketi kutoka kulia ni mkuu wa wilaya ya Iramba,Yahaya Nawanda na Mstahiki Meya wa manispaa ya Singida,Sheikh Salumu Mahami.
 Mkuu wa wilaya ya Iramba mkoa wa Singida,Yahaya Nawanda, akitoa mada yake iliyohusu mfuko wa afya ya jamii (CHF) kwenye mkutano wa wadau wa afya wa manispaa ya Singida.
Mkuu wa wilaya ya Singida,Queen  Mlozi,(wa kwanza kulia) akisikiliza mada zilizokuwa zikitolewa kwenye mkutano wa wadau wa afya wa manispaa ya Singida. Wa kwanza kushoto,ni mstahiki meya wa manispaa ya Singida,Sheikh Mahami.
Mkuu wa mkoa wa Singida,Dk.Parseko Kone (wa tatu kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na madiwani wa manispaa ya Singida.Walioketi wa  kwanza kulia ni Diwani wa viti maalum Yagi Kiaratu na anayefuatia ni mstahiki Meya wa manispaa ya Singida,Sheikh Salum Mahami.Kulia ni Katibu Tawala mkoa wa Singida,Liana Hassan mkuu wa wilaya ya Iramba,Yahaya Nawanda na mkuu wa wilaya ya Iramba na Queen Mlozi, mkuu wa wilaya ya Singida.

WADAU wa afya katika Halmashauri ya Manispaa ya Singida kwa kauli moja wameridhia kuanzishwa kwa Mpango wa Tiba kwa Kadi (TIKA) katika Manispaa hiyo.

 Wadau hao wamefikia uamuzi huo baada ya kubaini kuwa mpango wa TIKA una manufaa mengi ikiwemo mwananchi baada ya kulipa ada ya uanachama, atakuwa na haki ya kupata huduma za matibabu ndani ya Manispaa kwa mwaka mzima.

 Kwa mujibu wa Meneja Msaidizi wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) Mkoani Singida, Isaya Shekifu mpango wa TIKA ambao unafafana na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) unatumika mijini tu.

 Shekifu amesema uanachama wa TIKA ni wa mtu mmoja mmoja, wakati ule wa CHF, ni wa familia au kikundi.

 “Kwa sasa hapa Manispaa ya Singida, baada ya mpango huo kupata baraka ya kuanzishwa tunaendelea na mchakato wa kubadilisha sheria ndogo ya CHF kwenda kwenye Tiba kwa Kadi (TIKA)”,alifafanua Shekifu.

 Meneja Msaidizi huyo amesema baada ya kukamilika kwa sheria ndogo itakayotawala uendeshaji wa TIKA, mpango huo utaanza rasmi mapema iwezekanavyo mwaka huu.

 Akizindua mpango huo wa Tiba kwa Kadi (TIKA) katika Manispaa ya Singida juzi, Mkuu wa Mkoa wa Singida, Dk. Parseko Kone amesema mpango wa TIKA utawahakikisha wakazi wa Manispaa ya Singida na viunga vyake  mwanzo mpya wa kupata huduma za matibabu zenye uhakika.

 Hata hivyo, Dk. Kone aliagiza  viwango vya uchangiaji vya TIKA zitazingatia uwezo wa mwananchi kulipia pia vitazingatia

hali ya sasa ya huduma za matibabu.

 Katika hatua nyingine, Mkuu huyo wa Mkoa amesema kwa kuwa suala la TIKA ni la hiari wananchi watajiunga  kwa wingi endapo  watahamasishwa kikamilifu.

 “Kila mmoja hapa awe balozi mzuri kwa kuhamasisha wannachi wajiunge na mpango huu mara baada ya sheria ndogo kupitishwa.  Manispaa ihakikishe huduma zinakuwa bora katika vituo vyote ikiwa ni pamoja na lugha nzuri kwa wananchama”,amesema Dk.Kone.

No comments:

Post a Comment