Thursday, January 9, 2014

Mke amuua mume kwa kumpiga na kipande cha Mti Kichwani kisa Tsh. 25,000/=

Kamanda wa polisi mkoa wa Singida, SACP Geofrey Kamwela,akitoa taarifa kwa waandishi wa habari (hawapo kwenye picha) juu ya kifo cha Mwanaume aliyeuwawa na mkewe kwa kupigwa na kipande cha mti kichwani.

MKULIMA na Mkazi wa kijiji cha Ntewa, Kata ya Ntuntu tarafa ya Munghaa wilaya ya Ikungi mkoani Singida,Juma Abdallah (25) amefariki dunia baada ya kupigwa na mke wake Veronika Hamisi (25) kichwani katika paji la uso na na kufariki papo hapo.

Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Singida,SACP Geofrey Kamwela amesema tukio hilo limetokea januari  mbili mwaka huu saa saba mchana huko katika kijiji cha Ntewa.

Amesema siku ya tukio katika muda huo wa saa saba mchana wanandoa hao walirejea nyumbani kwao wakitokea kwenye klabu cha pombe za kienyeji aina ya mtukuru.

“Wanandoa hao vijana wakiwa nyumbani kwao,Juma alichukua pochi ya mke wake Veronica na kuchukua bila idhini shilingi 25,000 zilizokuwa zimehifadhiwa kwenye pochi hiyo”,amesema.

Kamanda Kamwela amesema baada ya Juma kuchukua fedha hizo bila idhini mke wake alimsihi sana azirudishe fedha hizo mahali zilipokuwa lakini juhudi hizo hazikuzaa matunda.

“Hata hivyo,Veronica alipoona juhudi zake zimegonga mwamba aliita wanaume wawili ambao majina yao hayajajulikana.Wanaume hao walipomshika Juma hapo ndipo Veronica alipopata fursa ya kuchukua kipande cha mti na

kumpiga mume wake na kusababisha kifo chake”,alifafanua Kamwela.

Amesema wanaume hao baada ya kuona Juma amefariki dunia haraka walikimbilia kusikojulikana Juhudi zaidi zinaendelea ili waweze kukamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.Veronica tayari anashikiliwa na polisi.

No comments:

Post a Comment